Na. Shinyanga RS.
MKUU wa Wilaya ya Kishapu Mhe. Joseph Mkude amezindua zoezi la uwekaji alama kwenye mipaka ya vyanzo vya maji katika Bwawa la Songwa na Mhumbu yaliyopo wilaya ya kishapu kwa lengo kuvilinda vyanzo vya maji na kuzuia shughuli za kibinadamu huku akiwasisizitiza wananchi waishio jirani na maeneo hayo kuendelea kupanda miti na kutunza mazingira.
Mhe. Mkude pamoja na mambo mengine lakini pia ametoa wito kwa wananchi wasifanye shughuli za kibinadamu kwenye mabwawa haya ikiwamo na kufanya shughuli za kilimo na uchimbaji madini, bali wavitunze vyanzo hivyo vya maji kwa faida yao na vizazi vijavyo.
“Natoa wito kwa wananchi vitunzeni vyanzo hivi vya maji msifanye kabisa shughuli za kibinadamu, na katika Mabwawa haya yamejengwa Matangi kwa ajili ya kunyweshea mifugo yatumieni na msiingize tena mifugo ndani ya maji,”amesema Mkude.
Awali akimkaribisha Mkuu wa Wilaya, Mhandisi wa Mazingira kutoka Bodi ya Maji Bonde la Kati Nyacheli Mramba, amesema wameweka alama hizi za mipaka na mabango ili kuzuia wananchi wasifanye shughuli za kibinadamu kwenye vyanzo hivyo ili kuvilinda visitoweke.
Katika hatua nyingine, amewataka wananchi wa Kishapu kuzitumia ipasavyo Mvua ambazo zinanyesha hivi sasa, kwa kupanda miti ili kuifanya Kishapu kuwa ya kijana.
Kwa upande wao wananchi wa Kata ya Songwa wamesema uwekaji huo wa alama za mipaka katika mabwawa haya utasaidia kuvilinda vyanzo hivyo vya maji ambavyo vilikuwa hatarini kutoweka, kutokana na shughuli za kibinadamu ikiwamo kilimo, uvuvi na uchimbaji madini na kuahidi kuwa watatekeleza maelekezo yote yaliyotolewa na viongozi.
Boma Street, Mwanza Road
Anuani: P.O.Box 320, Shinyanga
Simu: +255 28 2762222
Simu ya Mkononi:
Barua Pepe: ras@shinyanga.go.tz
Hakimiliki@2018. Mkoa wa Shinyanga. Haki zote zimehifadhiwa