Na Paul Kasembo – USHETU,
Kampuni ya Ujenzi ya NUSAK COMPANY LTD imeipongeza Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mhe. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuendelea kuwathamini, kuwatambua na kuwaamini wakandarasi wazawa, hatua inayowezesha kampuni hizo kushiriki kikamilifu katika miradi mbalimbali ya maendeleo nchini.
Akizungumza wakati wa ukaguzi wa maendeleo ya ujenzi wa Shule ya Sekondari ya Amali ya Mkoa inayojengwa katika Halmashauri ya Wilaya ya Ushetu, Mkurugenzi wa NUSAK CO. LTD, Ndg. Nurdini Said Kindamba, alimshukuru Mhe. Rais kwa msimamo thabiti wa Serikali katika kuwaamini na kuwawezesha wakandarasi wazawa kushiriki katika utekelezaji wa miradi mikubwa ya maendeleo.
"Kwa dhati tunamshukuru sana Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan na Serikali yake kwa kutuamini na kutupa fursa ya kushiriki katika miradi ya kimkakati kama huu wa ujenzi wa Sekondari ya Amali. Hii ni ishara ya wazi kuwa Serikali inathamini uwezo wa wazawa katika kuchangia maendeleo ya nchi," alisema Kindamba.
Naye Meneja Mradi wa ujenzi huo, Eng. Khamisi Ngonde, alieleza kuwa kampuni imeongeza nguvu kazi na masaa ya kazi ili kuhakikisha ujenzi huo unakamilika kwa wakati, kwa kuzingatia ubora na masharti ya mkataba bila kuongeza gharama yoyote, kama sehemu ya kuunga mkono jitihada za Serikali ya Mkoa na Taifa kwa ujumla.
Kando na pongezi hizo, elimu ya amali imetajwa kuwa nyenzo muhimu katika kukuza ujuzi wa vitendo kwa vijana katika maeneo mbalimbali kama vile ufundi, kilimo, uvuvi, sanaa na michezo. Serikali inahimiza wazazi, walezi na wawekezaji kushirikiana katika kuimarisha elimu hiyo kama njia ya kukabiliana na changamoto ya ajira na kuongeza ufanisi katika sekta ya uzalishaji.
NUSAK pia imempongeza Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Mhe. Anamringi Macha na Mkuu wa Wilaya ya Kahama Mhe. Mboni Mhita kwa usimamizi na mchango wao mkubwa katika kuhakikisha utekelezaji wa miradi ya maendeleo unakwenda sambamba na dira na maono ya Mhe.Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kuwaletea wananchi maendeleo ya haraka na ya kweli.
Boma Street, Mwanza Road
Anuani: P.O.Box 320, Shinyanga
Simu: +255 28 2762222
Simu ya Mkononi:
Barua Pepe: ras@shinyanga.go.tz
Hakimiliki@2018. Mkoa wa Shinyanga. Haki zote zimehifadhiwa