#shinyanga_rs
Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Mkoa wa Shinyanga imeanza kuchukua hatua dhidi ya wote waliobainika kuhusika na ubadhirifu wa fedha zaidi ya shilingi milioni 92 zilizotengwa kwa ajili ya kuwafidia wakulima wa tumbaku kupitia Chama cha Msingi cha Ushirika (AMCOS) Ibambala kilichopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Ushetu.
Akizungumza na waandishi wa habari Mei 27, 2025 mjini Shinyanga, Mkuu wa TAKUKURU mkoani humo, Bw. Donasian Kessy, amesema kuwa fedha hizo zilitolewa kwa ajili ya kuwasaidia wakulima waliopata hasara kufuatia mafuriko katika msimu wa kilimo wa mwaka 2023/2024. Hata hivyo, hazikuwafikia walengwa kama ilivyokusudiwa.
“TAKUKURU tumeanza kuchukua hatua kwa wote waliohusika na ubadhirifu wa shilingi zaidi ya milioni 92 zilizotengwa kwa ajili ya kuwafidia wakulima wa tumbaku wa AMCOS Ibambala,” alisema Bw. Kessy.
Kwa mujibu wa Bw. Kessy, katika kipindi cha Januari hadi Machi 2025, TAKUKURU Mkoa wa Shinyanga ilipokea jumla ya taarifa 57 za tuhuma za rushwa. Kati ya hizo, taarifa 52 zilifanyiwa uchunguzi na 13 zimefikishwa mahakamani.
Katika kipindi hicho, TAKUKURU pia imefanya mikutano ya hadhara 61, semina 30, na vipindi 13 vya elimu kwa umma kupitia vituo mbalimbali vya redio na runinga, kupitia programu ya Takukuru Rafiki, ikiwa ni sehemu ya juhudi za kuelimisha umma kuhusu mapambano dhidi ya rushwa.
TAKUKURU inatoa wito kwa wananchi kuendelea kushirikiana na taasisi hiyo kwa kutoa taarifa za vitendo vya rushwa kupitia simu ya bure 113 au kwa kutembelea tovuti rasmi ya taasisi hiyo: www.pccb.go.tz.
Boma Street, Mwanza Road
Anuani: P.O.Box 320, Shinyanga
Simu: +255 28 2762222
Simu ya Mkononi:
Barua Pepe: ras@shinyanga.go.tz
Hakimiliki@2018. Mkoa wa Shinyanga. Haki zote zimehifadhiwa