Na. P.aul Kasembo.
Mkurugenzi wa Daftari na Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) kutoka Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi (INEC), Ndg. Stanslaus Mwita, amesema kuwa wamefika kujiridhisha kama taratibu na mchakato mzima wa mgawanyo wa Jimbo la Solwa ulifuatwa kulingana na maelekezo waliyotoa awali kabla ya kuanzishwa kwa zoezi hilo.
Stanslaus aliyasema hayo Aprili 23, 2025, wakati akiwasilisha taarifa ya INEC kwa wadau wa uchaguzi katika ukumbi wa mikutano uliopo kwenye jengo la Utawala la Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga. Kikao hicho kilihudhuriwa pia na Makamu Mwenyekiti wa INEC, Mhe. Jaji wa Rufaa (Mstaafu) Mbarouk Salim Mbarouk, Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga Mhe. Anamringi Macha, na Katibu Tawala wa Mkoa huo, CP Salum Hamduni.
Wengine waliohudhuria ni Mkuu wa Wilaya ya Kishapu, Mheshimiwa Peter Masindi (aliyemwakilisha Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga, Mhe. Julius Mtatiro - Wakili), Mraribu wa Uandikishaji Mkoa wa Shinyanga Ndg. Bakari Kasinyo, Waheshimiwa Madiwani, Viongozi wa Dini, Viongozi wa Vyama vya Siasa pamoja na wataalamu mbalimbali wakiongozwa na Mkurugenzi wa Shinyanga DC Dkt. Kalekwa Kasanga.
"Tumekuja kujiridhisha na kuona kama taratibu na mchakato mzima wa mgawanyo wa Jimbo la Solwa ulifuatwa kulingana na maelekezo tuliyotoa kama INEC hapo awali kabla ya kuanzishwa kwa jambo hili. Hii ni sehemu tu ya mchakato, na si kwamba Tume imeridhia rasmi," alisema Mwita.
Awali, akitoa salamu za INEC, Makamu Mwenyekiti Mhe. Jaji wa Rufaa (Mstaafu) Mbarouk Salim Mbarouk alisema kuwa, pamoja na mambo mengine, uchambuzi wa kina ulifanyika kuhusu ombi hilo kwa kuzingatia vigezo muhimu ikiwemo kufanyika kwa vikao halali vya kisheria, idadi ya watu, mipaka ya kijiografia ya Jimbo la Uchaguzi, jina la Jimbo pamoja na mgawanyo wa Kata.
Nao wadau wa uchaguzi wa Shinyanga DC, akiwemo Katibu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) wa Jimbo la Solwa, Ndg. Mashindike Bulanya, waliishukuru INEC kwa kuja kujiridhisha na kwamba, utekelezaji wa ugawaji wa Jimbo la Solwa unalenga kurahisisha utoaji huduma kwa wananchi.
Boma Street, Mwanza Road
Anuani: P.O.Box 320, Shinyanga
Simu: +255 28 2762222
Simu ya Mkononi:
Barua Pepe: ras@shinyanga.go.tz
Hakimiliki@2018. Mkoa wa Shinyanga. Haki zote zimehifadhiwa