Na. Paul Kasembo, SHY RS.
Mrajisi Msaidizi wa Vyama Vikuu vya Ushirika Mkoa wa Shinyanga Ndg. Kakozi Ibrahim amekitaka Chama cha Ushirika Mkoa wa Shinyanga (SHIRECU) 1984 LTD kuweka kipaumbele na kuhakikisha wanajisajili na kutumia mifumo ya kidigitali ili kuendesha Chama kibiashara zaidi pamoja na kushirikiana na wadau mbalimbali katika shughuli za uzalishaji na biashara kwa maslani mapana ya Chama.
Ameyasema haya Machi 28, 2025 wakati akifungua Mkutano Mkuu wa 30 wa SHIRECU uliofanyika kwenye Ukumbi wa Mikutano wa SHIRECU uliopo Manispaa ya Shinyanga ambapo pamoja na yote ameongeza kuwa Tume ya Maendeleo ya Ushirika (TCDC) inasisitiza Vyama vya Ushirika kuwa na akaunti za Benki katika Benki ya Maendeleo ya Ushirika ikiwa ni sehemu ya kuhamasisha matumizi ya mifumo ya kidigitali katika uboreshaji wa vyama.
“Pamoja na kuwapongeza kwa jitihada mnazofanya lakini ninawasisitiza kuweka kipaumbele cha kuhakikisha mnajisajili na kutumia mifumo ya kidigitali ili kuendesha chama kidigitali na kibiashara zaidi sambamba na kushirikiana pamoja na wadau mbalimbali katika shughuli za uzalishaji na biashara kwa maslahi ya kufanya chama kisonge mbele zaidi,” amesema Ndg. Ibrahim.
Kwa upande wake Kaimu Meneja Mkuu wa SHIRECU Bi. Asnath Changamike akiwasilisha taarifa ya Utekelezaji ya Bodi amesema kuwa kuanzia Aprili 2024 hadi kufikia Machi 2025 chama kimefanikiwa kukusanya takribani Tzs. Bilioni 1 ambayo ni sawa na asilimia 68.61 ya ukusanyaji wa mapato kupitia shughuli za ndani za chama.
Aidha ameongeza kuwa SHIRECU imefanikiwa pia kusajili Vyama vya Ushirika wa Kilimo na Masoko (AMCOS) takribani 127 pamoja na kusajili wanachama wapatao elfu 30 kwenye Mfumo wa Kielekroniki wa Usimamizi wa Vyama vya Ushirika (MUVU) ili kuwaunganisha ili kuwa na ukaribu kupitia mifumo hiyo ya kidigitali.
Mkutano Mkuu wa 30 wa SHIRECU 1984 LTD pamoja na mambo mengine umejadili, kupokea na kuhuisha sera mbalimbali za Ushirika, kujadili na kupitisha ukomo wa madeni sambamba na kupokea taarifa ya utekelezaji ya Bodi na kupitisha bajeti ya chama kwa mwaka wa fedha 2025/2026.
Boma Street, Mwanza Road
Anuani: P.O.Box 320, Shinyanga
Simu: +255 28 2762222
Simu ya Mkononi:
Barua Pepe: ras@shinyanga.go.tz
Hakimiliki@2018. Mkoa wa Shinyanga. Haki zote zimehifadhiwa