Na. Paul Kasembo, SHY RS.
MRATIBU wa Michezo ya Jadi Tanzania (CHAMIJATA) ndugu Abubakary Kyaibamba amesema kuwa michezo ya jadi ni ajira kama zilivyo ajira nyingine na pia ni utambulisho rasmi wa jamii flani mbele ya jamii nyingine.
Abubakary ameyasema hayo leo tarehe 24 Machi, 2025 wakati akizungumza na wajumbe wa Kamati Tendaji ngazi ya Wilaya na Mkoa kikao ambacho kilifanyika katika ukumbi wa mikutano uliopo Ofisi ya Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga huku Bi. Janeth Elias ambaye ni Afisa Utamaduni kutoka Ofisi ya Mkuu wa Mkoa akipongeza uwepo wa kikao hicho na kwamba kinakuja kurejesha uhai wa michezo hiyo.
Abubakary alisema kuwa michezo ya jadi kama ilivyowekewa msisitizo na Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan na Serikali yake inakuja na utambuzi wa jamii, kuongeza ajira, kuimarisha utamaduni na mila zetu ambapo kwa Mkoa wa Shinyanga wenyeji wanautambua kama (MBINA) ni mchezo maarufu na mchezo pendwa zaidi kwa kabila la Wasukuma.
"Ndugu zangu wajumbe, michezo ya jadi ni ajira kwa vijana na utambulisho wa jamii flani mbele ya jamii nyingine kwakuwa unakuwa na tamaduni, mila na desturi zake tofauti na nyingine lakini pia inatumika kama sehemu ya ajira katika sehemu mbalimbali za burudani na michezo ambayo hukutanisha watu wengi na kuongeza mzunguko wa uchumi kwa eneo husika," alisema Abubakary.
Ujio wa CHAMIJATA mkoani Shinyanga unalenga kuchechemua, kurejesha hamasa ya mchezo huo ambapo kwa miaka ya hivi karibuni umebakiwa ukichezwa na kuadhimishwa katika sherehe za SANJO YA BUSIYA @busiyachiefdom ambayo hufanyika katika Kata ya Ukenyenge, Wilaya ya Kishapu katika viwanja vya Utemini maarufu kama BUSIYA CHIEFDOM kila ifikapo Julai ya kila mwaka.
CHAMIJATA pamoja na mambo mengine inakuja na mkakati wa kuibua vipaji zaidi kwa vijana ili waweze kuiheshimisha michezo ya jadi kama ilivyokuwa hapo awali ambapo sasa watacheza, kuenzi na kuwaunganishwa pamoja kupitia michezo hiyo jambo ambalo litaipelekea kuimarika zaidi kwa amani, upendo na mshikamano miongoni mwa jamii huku ikitajwa kuwa ni michezo ambayo haukipewa kipaumbele miaka ya hivi karibuni.
Boma Street, Mwanza Road
Anuani: P.O.Box 320, Shinyanga
Simu: +255 28 2762222
Simu ya Mkononi:
Barua Pepe: ras@shinyanga.go.tz
Hakimiliki@2018. Mkoa wa Shinyanga. Haki zote zimehifadhiwa