#shinyanga_rs
Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga Mhe. Julius Mtatiro (Wakili) @julius_mtatiro amewataka Wanavikundi ambao wamepokea Mikopo ya asilimia 10 ya Wanawake, Vijana na Watu wenye Ulemavu kutoka Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga kuitumia mikopo hiyo kwenye Miradi waliokusudia wakati wanaomba mikopo huku akiwasihi wairejeshe mikopo hiyo kwa wakati kwani mikopo hii ni ya hiari lakini urejeshaji ni lazima.
DC Mtatiro ameyasema haya leo Aprili 2, 2025 kwenye Hafla ya utoaji mkopo kwa vikundi vya Wanawake, Vijana na Watu wenye Ulemavu, hafla iliyofanyika kwenye Viwanja vya Soko Kuu la Manispaa ya Shinyanga ambapo pamoja na yote amempongeza Mkurugenzi wa Manispaa Mwl. Alexius Kagunze, Katibu Tawala na Meya wa Manispaa ya Shinyanga kwa ukusanyaji mzuri wa mapato ambayo yanasaidia katika uwezeshaji na utoaji wa mikopo hii ambayo inawanufaisha na kuwawezesha wananchi kiuchumi.
“Ninawasisitiza wanavikundi ambao mmepata mikopo hii mkaitumie kwenye miradi ambayo mlikusudia kipindi mnaomba mikopo na msijaribu kuzitumia fedha hizo kwenye miradi mingine ambayo hamkuiorodhesha kwani kufanya hivyo ni kinyume cha kanuni na taratibu, lakini pia ninawasihi muirejeshe mikopo hii kwa wakati kulingana na muda ambao umewekwa kwani kukopa ni hiari lakini kurejesha ni lazima” amesema DC Mtatiro.
Aidha DC Mtatiro amewasihi wanavikundi ambao wamepata mikopo hii kuwasiliana na Maafisa Maendeleo ngazi ya Kata na katika maeneo wanayoishi kwa ukaribu pindi wanapopata changamoto kwenye urejeshaji wa mikopo ili waweze kusaidiwa na kutafuta suluhu za changamoto ambazo huenda wakapitia badala ya kusubiri mpaka watafutwe pindi wanaposhindwa kurejesha.
Kwa upande Kaimu Mkurugenzi wa Manispaa ya Shinyanga Ndg. Peres Kamugisha akiwasilisha taarifa ya utoaji wa mikopo ya asilimia 10 kwa Wanawake, Vijana na Watu wenye Ulemavu amesema mpaka sasa wametoa takribani Mil. 255 kwenye Vikundi 19 ambapo 11 ni vya Wanawake, 7 vya Vijana na Kikundi 1 cha Walemavu huku akiendelea kusisitiza kuwa mikopo hii ni endelevu na itaendelea kutolewa kwenye vikundi ambavyo vitakidhi kanuni na taratibu.
Boma Street, Mwanza Road
Anuani: P.O.Box 320, Shinyanga
Simu: +255 28 2762222
Simu ya Mkononi:
Barua Pepe: ras@shinyanga.go.tz
Hakimiliki@2018. Mkoa wa Shinyanga. Haki zote zimehifadhiwa